Vuta ni kuvute baina ya wajumbe wa Baraza la Usalama kuhusu sakata la madai ya matumizi ya silaha za kemikali huko Douma nchini Syria, imeendelea hii leo baada ya maazimio mawili tofauti yaliyowasilishwa mbele yao mchana wa leo Jumanne kugonga mwamba.
Azimio moja liliwasilishwa na Marekani likilenga kuanzisha jopo huru la Umoja wa Mataifa la kuchunguza matumizi ya silaha za kemikali huko Syria, ilhali azimio lingine liliwasilishwa na Urusi likilenga kuondoa ombwe la uchunguzi lililoibuka baada ya jopo la awali la uchunguzi huko Syria kutoongezewa muda.