Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Adhabu ya kifo haitapunguza ugaidi: Ban

Adhabu ya kifo haitapunguza ugaidi: Ban

Leo ni siku ya kupinga hukumu ya kifo duniani ikiangazia matumizi yake dhidi ya ugaidi ambapo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amesema hukumu ya kifo ni zoezi la kikatili na la kinyama na haina nafasi katika karne hii.

Amesema adhabu hiyo ambayo sasa inatumika kwa kiasi kikubwa katika kupambana na ugaidi mara nyingi haifuati sheria, na hufanyika pasipo na ufanisi na hivyo si halali, na badala ya kupunguza ugaidi vinachochea zaidi tatizo hili.

Katika ujumbe wake wa siku hii Ban ameongeza kuwa hivi karibuni wahanga wa hukumu hiyo wamekuwa ni watu wanaotumia haki zao za kiraia kama kuandamana, kujieleza katika mitandao ya kijamii ama vyombo vya habari, ama wapinzani wa serikali na amekumbusha kwamba vitendo hivyo si uhalifu wala vitendo vya kigaidi.

Kwa mantiki hiyo ametoa wito kwa nchi 65 duniani ambazo bado zinatumia hukumu ya kifo kukomesha adhabu hii katika nyanja zote.

Vile vile katika ujumbe wao, wataalamu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa pia wamezikumbusha serikali kote duniani, kwamba, hukumu ya kifo haipaswi kutumika katika kupambana na ugaidi na halihalalishi kukiuka viwango vya kimataifa vya kulinda haki za binadamu.