Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Afisa wa UM kuhusu amani na usalama azuru Burundi

Afisa wa UM kuhusu amani na usalama azuru Burundi

Mwenyekiti  wa Kitengo  cha kuimarisha amani na usalama katika umoja wa mataifa yuko ziarani nchini Burundi. Bwana  Jurg Lauber  ambaye pia ni balozi wa Uswisi kwenye Umoja wa Mataifa amekutana  kwa mazungumzo na Rais wa Burundi Pierre Nkurunziza  katika  juhudi za kumaliza mgogoro wa kisiasa nchini humo na kuinua uchumi wa nchi hiyo ulioathirika kutokana na ghasia zilizodumu kwa zaidi ya miezi 10.

Wakati  huo huo, Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anayehusika na maswala ya haki za binaadamu Ivan  Simonovic ameanza ziara nchini humo kutathimini hali ya haki za binadaamu  na kuandaa ziara ya Katibu Mkuu  wa Umoja wa mataifa Ban Ki-moon baadaye mwezi  huu.Kutoka Bujumbura, Mwandishi wetu Ramadhani KIBUGA anasimulia zaidi.

(TAARIFA YA KIBUGA)

Mwenyejiti wa  Kitengo cha kuimarisha amani  na usalama katika  Umoja  wa Mataifa  anayehusika na Burundi  ambaye pia  ni Balozi wa Uswisi kwenye  shirika hilo  Jurg Lauber amesema shabaha ya ziara yake ni kutathimi hali halisi  ya usalama Burundi na njia za kukwamua  mgogoro lakini pia kuinua uchumi wa taifa kama alivyosema muda mfupi baada ya kupokelewa kwa mazungumzo na Rais wa burundi Pierre Nkurunziza.

(SAUTI YA JURG LAUBER)

“Tumezungumzia kuhusu hali ya usalama nchini, kuhusu mazingira ya mazungumzo ya kisiasa ndani ya nchi na kuhusu hasa   hali ya kiuchumi. Nimetilia hasa mkazo kuhusu hali ya uchumi kwenye mazungumzo yangu na rais , kama mnavojuwa  uchumi umeathirika zaidi kutokana na mgogoro wa kisiasa unaoisibu Burundi tangu mwaka jana na ambao unaendelea na tumezungumzia uwezekano wa kupanua ushirikiano zaidi kati ya burundi na Umoja wa Mataifa na kitengo hiki pamoja na zingine idara za Umoja wa mataifa ili kuinua hali ya uchumi wa nchi “

Kwa mujibu wa Naibu msemaji wa Rais wa Burundi Claude Karegwa, Rais Nkurunziza amesifu mchango wa  Umoja wa Mataifa .

(SAUTI YA KAREGWA)

“Rais amempongeza kuhusu juhuzi zinazofanywa na Umoja wa mataifa kusaidia Burundi na kumuhakikishia kuwa serikali ya Burundi kama inavoombwa  itafanya kila iwezalo ili kuimarisha amani  na usalama nchini pamoja na kutunisha uchumi wa taifa ili kustaawisha wananchi. Rais pia ameutaka Umoja wa Mataifa  wasaidie kutoa msukumo ili Tume ya Ukweli na Mariadhiano ifanye kazi maana shughuli za tume hiyo ndio itakamilisha mpango wa amani."