Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

FAO yataka hatua zichukuliwe kudhibiti matumizi ya dawa za kuua vijiumbemaradhi

FAO yataka hatua zichukuliwe kudhibiti matumizi ya dawa za kuua vijiumbemaradhi

Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Chakula na Kilimo (FAO), Helena Semedo ametaka hatua ya kimataifa kukabiliana na athari ya dawa za kuua vijiumbemaradhi hasa kwa usalama wa chakula na afya katika nchi za kipato cha chini. John Kibego na Taarifa Kamili.

(TAARIFA YA KIBEGO)

Akihutubia mawaziri wa Ulaya wa afya na kilimo kwenye mkutano mjini Amsterdam, Bi Semedo amezingatia haja ya ushirikiano wa kimataifa kukabiliana na changamoto hii, kutokana na jinsi dawa za kuua vijiumbemaradhi zinavyohatarisha afya na usalama wa chakula.

Amesema, matumizi mabaya na kwa muda mrefu ya dawa hizo huongeza uhimili wa bakteria ambazo dawa hizo zilitengenezwa kuangamiza, akisema, matumizi hayo yanarudisha nyuma hatua zilizopigwa katika karne moja.

Ikiwa udhibiti wa magonjwa ni miongoni mwa changamoto kubwa duniani, sanjari na mabadiliko ya tabianchi na ukuwaji wa maeneo ya mijini, Bi. Semedo amesema, madhara ya dawa hizi huenda ni zaidi kwa mwanadamu na aina nyingi za wanyama wengine. Juan Lubroth, ni Afisa Mkuu wa afya ya mifugo, FAO.

"Ni jukumu la nani?  sisi sote tuna jukumu, kama mgonjwa, ni lazima umalize dozi yote ya viuavijasumu au antibayotiki uliyoandikiwa na daktari hata kama unajisikia vizuri. Na kama daktari ni lazima utambuzi uwe sahihi na kutoa viuavijasumu  sahihi kwa mgonjwa, na kwa mtengenezaji ni muhimu kwako kuwa na usimamizi mzuri ambapo chanjo zitawakinga  vyema wanyama dhidi ya magonjwa na hautalazimika kutumia viuavijasumu."