Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban Ki-moon aendelea kuwa na wasiwasi kuhusu Burundi

Ban Ki-moon aendelea kuwa na wasiwasi kuhusu Burundi

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon anaendelea kufuatilia mzozo wa kisiasa nchini Burundi akiwa na wasiwasi kuwa mzozo huo unaweza kuharibu mwongo mmoja wa jitihada za kujenga amani na maridhiano nchini humo.

Taarifa iliyotolewa leo na msemaji wake inasema kwamba Katibu Mkuu amekaribisha mapendekezo yaliyotangzwa na Muungano wa Afrika baada ya mkutano wa viongozi wa tarehe 13 Juni kuhusu jinsi ya kuandaa uchaguzi wenye amani nchini humo.

Aidha Ban Ki-moon amesema mwakilishi wake maalum na mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa kwa ukanda wa Afrika ya Kati, Abdoulaye Bathily, ataenda Burundi tarehe 21 Juni kusaidia Burundi kupunguza mvutano na kutatua mzozo. Bwana Bathily atashirikiana na Muungano wa Afrika, Jumuiya ya Afrika ya Mashariki, na mkutano wa kimataifa wa maziwa makuu, ICGLR.

Halikadhalika bwana Ban amemshukuru Mjumbe wake maalum Said Djinnit kwa juhudi zake katika kuhamasisha mazungumzo baina ya wadau wa Burundi mwezi Mei na Juni mwaka huu.

Hatimaye amewasihi viongozi wa Burundi kuwajibika na kuanzisha upya mazungumzo ya kisiasa ili kuandaa uchuguzi jumuishi wenye amani.