Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Waasi wa LRA bado ni tishio ukanda wa Afrika ya Kati: UNOCA

Waasi wa LRA bado ni tishio ukanda wa Afrika ya Kati: UNOCA

Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa leo limeelezwa kuwa ukanda wa Afrika ya Kati umeendelea kukumbwa na matukio yanayoathiri usalama wa eneo hilo ikitaja kikundi cha waasi cha Lord’s Resistance Army, LRA, biashara haramu ya mazao ya porini na mashambulio kutoka kwa magaidi wa Boko Haram.

Ripoti hiyo ni kwa mujibu wa Mkuu wa ofisi ya Umoja wa Mataifa kwa ukanda huo, UNOCA, Abdoulaye Bathily aliyotoa alipohutubia baraza hilo akisema mashambulio hayo yanaleta matatizo kama vile Jamhuri ya Afrika ya Kati na hata Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

Bwana Bathily amesema tangu ripoti yake mbele ya baraza hilo mwezi Novemba mwaka jana, hali imezidi kudorora kila uchao na kutia hofu.

(Sauti ya Abdoulaye)

"Nchi za Afrika ya Kati imeingia katika ng’we ya uchaguzi inayomalizika mwaka 2018. Mvutano wa kisiasa kuelekea chaguzi unaongezeka kwenye baadhi ya nchi. Masuala ya marekebisho ya katiba kuhusiana na ukomo wa uongozi yanagawa wapiga kura. Mivutano iandamanayo na ghasia  na kusababisha vifo mathalani DR Congo na Burundi. Malalamiki ya kijamii yanashika kasi, yakichochewa na kunywea kwa uchumi kwenye ukanda huo hasa nchi zinazozalisha mafuta.”

Kufuatia taarifa hiyo, Baraza la usalama limepitisha taarifa inayoshutumu mashambulio likisema  yanasikitisha na kwamba yanaweza kuwa uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya ubinadamu.

Halikadhalika baraza limeeleza wasiwasi wake kuhusu kuendelea kwa vitendo vya kigaidi vinavyochochewa na kundi la kigaidi la Boko Haram.