Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

WFP kupunguza mgao wa chakula kwa wakimbizi nchini Kenya

WFP kupunguza mgao wa chakula kwa wakimbizi nchini Kenya

Upungufu wa ufadhili na uhaba umelilazimu Shirika la Mpango wa Chakula Duniani, WFP kupunguza mgao wa chakula kwa wakimbizi nchini Kenya kwa asilimia 30.

Hii ni mara ya pili katika kipindi cha takriban miezi sita kwa shirika hilo kupunguza kiwango kinachopendekezwa cha mlo wa kila siku kwa wakimbizi hao, kwani liliwahi kufanya hivyo Novemba mwaka jana. Elisabeth Byrs ni msemaji wa WFP mjini Geneva

"Ni hali inayoleta hofu kubwa kwa WFP. Kwa sababu ya upungufu wa  fedha WFP sasa inalazimika kupunguza mgao wa chakula kwa baadhi ya wakimbizi Laki Tano , wengi wao wakiwa ni wasomali na waSudan Kusini, wanaoishi mashinani katika kambi ya Dadaab na Kakuma kaskazini mwa Kenya.”

WFP imesema inatumai kuwa hatua hii itadumu kwa muda mfupi tu, lakini huenda mgao huo utaendelea hadi Septemba. Imetoa wito kwa jamii ya kimataifa ichangie pengo la ufadhili la dola milioni 40 zinazohitajika hadi Januari mwakani.