Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wiki ya Afrika yaangazia ajenda ya 2063

nchini Uganda, picha ya UNDP Neil Palmer - CIAT

Wiki ya Afrika yaangazia ajenda ya 2063

Wakati maadhimisho ya wiki ya Afrika yakianza jumatatu tarehe 13 Oktoba katika Makao makuu ya Umoja wa Mataifa, Sam Kutesa, rais wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa amesema bara la Afrika ni sehemu inayovutia kwa biashara na uwekezaji. Taarifa zaidi na Priscilla Lecomte.

Sam Kutesa amesema lengo la ajenda ya maendeleo ya Afrika ifikapo 2063 ni kupata bara lenye maendeleo ya kiuchumi na usalama, akiongeza kwamba bara la Afrika limefanikiwa kuwa kwa kasi kukbwa kuliko sehemu nyingine za dunia, isipokuwa mashariki mwa Asia, kiwango cha ukuaji wa uchumi kikifikia asilimia 5.6 kwa kipindi cha miaka kumi iliyopita.

“Ajenda ya 2063 inasisitiza umuhimu wa Afrika yenye amani na usalama, ambapo maendeleo yanaendeshwa na raia wake wenyewe. Inatambua mchango wa wanawake na vijana. Inaangazia Afrika itakayowezesha maadili na mila za pamoja. Inatoa wito kwa Afrika itakayokuwa mdau mwenye nguvu katika maswala ya kimataifa”

Wiki ya Afrika imeadhimishwa na Umoja wa Mataifa pamoja na Muungano wa Afrika na mpango mpya wa ushirikiano wa maendeleo barani humo, NEPAD. Ajenda ya 2063 ni mpango wa maendeleo ya pamoja ulioandaliwa na Muungano wa Afrika