Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

WHO kuamua kuhusu Ebola

@WHO(Video capture)

WHO kuamua kuhusu Ebola

Shirika la afya duniani WHO litaitisha kikao cha kamati yake ya dharura kutathmini iwapo mlipuko wa ugonjwa wa Ebola huko Afrika Magharibi unaibua hofu ya kimataifa katika afya ya umma.

Mkutano huo huo utafanyika Jumatano na Alhamisi hii na ni mara ya kwanza kwa kamati hiyo kuitishwa kufanya uamuzi kuhusu Ebola, ugonjwa ambao tangu mwezi Machi mwaka huu umesababisha vifo vya watu 887 huko Guinea, Liberia, Sierra Leone na Nigeria.

Tarik Jasarevic ni msemaji wa WHO,Geneva.

(Sauti ya Tarik)

'Mkurugenzi mtendaji wa WHO anataka maoni ya kamati ya dharura ya iwapo  mlipuko wa ebola unaoshuhudiwa ni tishio kwa afya ya umma duniani. Iwapo ni tishio, basi kamati itapendekeza kwa Mkurugenzi mtendaji huyo kuwa WHO itangaze kuwa ni janga la afya ya umma na kutoa pendekezo la muda la jinsi ya kudhibiti kuenea kwake duniani.”

Kutokana na mlipuko huo, tayari WHO imeonya kuwa ugonjwa huo bado ni tisho na imezindua mpango wa hatua wenye thamani ya dola Milioni 100.

Hata hivyo hadi sasa WHO haijashauri zuio lolote la safari au kufungwa kwa mipaka kutokana na mlipuko wa Ebola huko Afrika Magharibi.