Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wajumbe heshimuni usiri wa mazungumzo epukeni kutia chumvi: Brahimi

Wajumbe heshimuni usiri wa mazungumzo epukeni kutia chumvi: Brahimi

Mjumbe wa pamoja wa Umoja wa Mataifa na Umoja wa nchi za kiarabu kwenye mzozo wa Syria, Lakhdar Brahimi ametaka wajumbe kwenye mazungumzo yanayoendelea huko Geneva Uswisi kuwa makini zaidi wanapozungumza na vyombo vya habari na kubwa zaidi ni kuheshimu usiri wa mazungumzo hayo.

Bwana Brahimi amewaambia waandishi wa  habari mjini Geneva kuwa hakuna tatizo la wajumbe wa pande mbili hizo kuzungumza na vyombo vya habari lakini kwa mtazamo wake anaona imepita kiasi.

(Sauti ya Brahimi)

Nimewaeleza mchana huu kuwa kuna umuhimu wa kuwajibika na kuheshimu usiri wa majadiliano na iwapo huheshimu usiri huo basi angalau usitie chumvi suala husika. Iwapo ni kweli kwamba mtu amesema upande wa serikali umesema mambo mabaya kuhusu dini na kwamba nimewakaripia, Si kweli! Kwanza kabisa mimi sikaripii mtu yeyote! Na hakukuwepo mambo mabaya yaliyosemwa kuhusu dini. Hivyo nimemtaka kila mmoja kuwa makini kiasi na taarifa za aina hiyo.”

Kwa mujibu wa Brahimi, asubuhi walijadili mada iliyowasilishwa na serikali kuhusu misingi mikuu ambayo kwa kiasi kikubwa imo kwenye tamko la Geneva. Amesema kesho watazugumzia tamko hilo na penginepo wanaweza kuanza mjadala.