Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mawaziri wa Utalii wataka uboreshaji wa sera kati ya utalii na usafiri wa angani

Mawaziri wa Utalii wataka uboreshaji wa sera kati ya utalii na usafiri wa angani

Mawaziri wa Utalii kutoka kote duniani wametaka uboreshwe utandawazi wa angani kwa kuweka uratibu mzuri wa sera za utalii na usafiri wa angani ili kuhakikisha ukuaji endelevu wa sekta hizo za utalii na usafiri wa angani. Hayo yamejitokeza katika mkutano wa kila mwaka wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Utalii Duniani, WTO na Shirika la Soko la Usafiri Duniani, WTM, ulofanyika mjini London, Uingereza.

Mkutano huo ulijadili masuala muhimu yanayohusiana na kuliziba pengo lililopo kisera kati ya sekta hizo mbili, ukiwemo mfumo uliopo sasa wa udhibiti, ushuru na hatma ya mfumo mzima wa usafiri.

Akiongea wakati wa mkutano huo, Katibu Mkuu wa WTO, Taleb Rifai, amesema ni dhahiri kuwa licha ya uhusiano wa kutegemeana kati ya usafiri wa angani na utalii, juhudi zaidi zinapaswa kuwekwa na sekta zote ili kubuni sera ya pamoja, ambayo italeta ushirikiano na ukuaji endelevu.

Washirika katika mkutano huo wamemulika teknolojia, ushirikiano wa umma na serikali, ushirikiano wa kikanda na uwekezaji katika miundo mbinu, pamoja na rasilmali ya watu, kama daraja la kuliziba pengo lililopo kisera kati ya utalii na usafiri wa angani, ili kuendeleza uwezaji wa usafiri.