UM uhakikishe biashara ya utumwa haijitokezi tena duniani –Dk Bana
Leo ni siku ya kimataifa ya kumbukumbu ya biashara ya utumwa na ukomeshaji wa biashara hiyo ambapo Umoja wa Mataifa huitumia siku hii kuwakumbusha watu madhila ya biashara ya utumwa katika bahari ya Atlantiki, sababu zake kihistoria, njia zilizotumika na hata madhara yake.
Akizungumzia siku hii Mkurugenzi Mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la elimu, sayansi na utamaduni Bi Irina Bokova amesema madhara ya historia ya bishara ya utumwa lazima yafahamike kwa wote kwa kufundishwa mashuleni, na kwingineko kupitia vyombo vya habari na kwamba UNESCO inawajibu wa kutimiza hilo kupitia walimu, kusaidia tafiti na kutunza utamaduni na urithi wa maandishi.
Naye mkuu wa idara ya sayansi ya siasa na utawala, ya chuo kikuu cha Dar es Salaam Dk Benson Bana katika mahojiano maalum na idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa amesema umoja wa Mataifa na jumuiya ya kimataifa zinawajibu wa kuhakikisha biashara hii haramu haijitokezi tena katika historia ya wanadamu na kuzungumzia pia umuhimu wa mgawanyo stahiki wa raslimali kama sehemu ya fidia ya biashara ya utumwa.
(SAUTI DK BANA)