Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wananchi katika jimbo la Jonglei Sudan Kusini wanaishi katika uoga: OCHA

Wananchi katika jimbo la Jonglei Sudan Kusini wanaishi katika uoga: OCHA

Mratibu wa masuala ya kibinadamu katika Sudan Kusini, Toby Lanzer, ametoa wito kwa serikali ya Sudan Kusini kuongeza nguvu juhudi zake za kuimarisha utiivu wa sheria na utaratibu, na kuwafikisha mbele ya sheria wale wote wanaotenda uhalifu na kuweka maisha ya watu hatarini.

Ametoa wito kwa makundi yote yenye silaha kuhakikisha ya kwamba raia hawalengwi wakati wa mapigano ya kijeshi, bila ubaguzi wa kikabila au eneo walipo.

Bwana Lanzer ameelezea wasiwasi wake kuhusu hatari inayoongezeka dhidi ya raia, akisema kuwa katika ziara yake hivi karibuni kwenye maeneo ya Akobo na Pibor, kwenye jimbo la Jonglei, alikutana na watu wanaoishi katika uoga na hali ya sintofahamu.