Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban aonyesha wasiwasi juu ya hatma ya kisiasa Maldives

Ban aonyesha wasiwasi juu ya hatma ya kisiasa Maldives

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon ameonyesha wasiwasi juu ya hali ya kisiasa huko Maldives na hatma ya rais wa zamani wa nchi hiyo Mohamed Nasheed ambaye kwa sasa ameomba hifadhi kwenye ubalozi wa India nchini humo. Bwana Ban amekaririwa na msemaji wake akipendekeza pande zote zinazovutana zijizuie kufanya vurugu na badala yake zishirikiane kumaliza mvutano nchini humo na kuweka mazingira stahili kwa uchaguzi ujao kwa mujibu wa katiba ya nchi hiyo. Nasheed amejihifadhi kwenye ubalozi wa India ulioko mji mkuu wa Maldives, Malé tangu tarehe 13 mwezi huu baada ya polisi kufanya jaribio la kumkamata kwa tuhuma kuwa enzi za uongozi wake alimtia rumande jaji mmoja kinyume cha sheria. Wafuasi wa Nasheed wanadai kuwa madai hayo yanalenga kumzuia asishiriki uchaguzi utakaofanyika mwezi Septemba mwaka huu.

Katibu Mkuu Ban ametaka kila chama kusimamisha mgombea wake wanaomtaka kwa kuzingatia utawala wa kisheria na katiba ya nchi hiyo.