Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Maelfu wapoteza makazi kufuatia mzozo Mali

Maelfu wapoteza makazi kufuatia mzozo Mali

Takribani watu Elfu Thelathini wanahofiwa kuwa wamepoteza makazi yao kutokana na mapigano huko maeneo ya Kati na kaskazini mwa Mali na inahofiwa kuwa idadi yao inaweza kuwa kubwa kwa kuwa vikundi vinavyodaiwa kuwa vya kiislamu vinazuia watu kukimbilia maeneo ya Kusini.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Msemaji wa Umoja wa Mataifa Eduardo del Buey wakati akizungumza na waandishi wa habari na kuongeza kuwa kuna ripoti za raia wa Mali kukimbilia nchi jirani.

“Wizara ya mambo ya ndani ya Mauritania imethibitisha kuwa maelfu wa watu wanakimbia Mali wakielekea mpaka wa Mauritania. Na hakuna idadi ya wakimbizi walioonekana wakiwasili Burkina Faso na Niger. Shirika la mpango wa chakula la Umoja wa mataifa, WFP linasema ukosefu wa usalama unafanya lishindwe kupeleka chakula maeneo ya kaskazini. Hata hivyo kwa msaada wa washirika wake limeweza kufikisha msaada wa dharura wa chakula kwa watu 270,000 wakiwemo wakimbizi wa ndani Elfu Sabini. WFP inatumia njia mbali mbali za usafiri ikiwemo boti ndogo kufikia Timbuktu kupitia mto Niger.”

Tangu mwezi Machi mwaka jana watu Laki Mbili na Elfu Thelathini wamekimbia makazi yao kutokana na mapigano na hofu ya usalama nchini Mali.