Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Bado Haiti inahitaji msaada: Ban

Bado Haiti inahitaji msaada: Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon ameomba jumuiya ya kimataifa kuendelea na moyo wa kusaidia Haiti katika ujenzi wa nchi yao baada ya tetemeko kubwa la ardhi miaka mitatu iliyopita lililosababisha vifo vya zaidi ya watu Laki Mbili.

Ban amesema hayo katika ujumbe uliosomwa kwa niaba yake na Mku uwa operesheni za ulinzi wa amani za Umoja wa Mataifa Hervé Ladsous, wakati wa kumbukumbu ya miaka mitatu ya tetemeko hilo huko Port au Prince, Haiti.

Pamoja na kukumbuka waliopoteza maisha wakiwemo wafanyakazi 102 wa Umoja wa Mataifa, Bwana Ban amesema kazi bado ni kubwa ya ujenzi huku akipongeza jitihada za serikali, washirika mbali mbali na moyo wa wananchi wenyewe wa Haiti katika ukarabati wa nchi yao.

Amesema hadi sasa bado zaidi ya watu Laki Tatu wanaishi kwenye makazi ya kuhamahama huku wakiwa wamekumbwa na vimbunga mfululizo vinavyowaweka katika maisha magumu zaidi ikiwemo kukosa uhakika wa chakula.