Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UM wahitaji dola Bilioni 8.5 kwa ajili ya misaada ya kibinadamu mwaka 2013

UM wahitaji dola Bilioni 8.5 kwa ajili ya misaada ya kibinadamu mwaka 2013

Umoja wa Mataifa umetangaza ombi la dola Bilioni 8.5 kwa ajili ya operesheni zake za misaada ya kibinadamu kwa mwaka 2013. Fedha hizo zinalenga kuwahudumia watu Milioni 51 kutoka nchi 16 duniani ambao wanahitaji misaada ya kibinadamu.

Katika usambazaji wa huduma hizo, jumla ya mashirika 520 ya misaada yatashirikiana na Umoja wa Mataifa kuwapatia misaada sambaza misaada kwa wakimbizi, watu waliopoteza makazi ndani ya nchi zao na makundi mengine yaliyo hatarini kutokana na kukumbwa na majanga ya kiasili na migogoro.

Akizungumza mjini Roma, Italia wakati wa uzinduzi wa ombi hilo la fedha, Mratibu Mkuu wa shughuli za misaada ya dharura kwa binadamu, Valerie Amos amesema bila kujali mdororo wa kiuchumi, jumuiya ya kimataifa inapaswa kuongeza juhudi kusaidia idadi kubwa ya watu waliojikuta wametumbukia kwenye majanga bila uamuzi wao.

Tunapoingia mwaka 2013, kasi ya mahitaji ya kibinadamu duniani haitapungua. Ombi letu linajumuisha mahitaji ya mamilioni ya wavulana na wasichana nchini Yemen ambao wanataabishwa na utapiamlo. Karibu Nusu milioni ya wakimbizi nchini Sudan Kusini na wale waliorejea nchini humo pamoja na watu wengine Milioni Mbili wanahitaji msaada wa chakula. Nchini Niger, watu Milioni Moja na Laki Saba hawana chakula cha kutosha. Tunaziomba serikali, watu binafsi na wafanyabiashara kuchangia kuokoa maisha ya watu mwaka 2013.”

Bi. Amos amesema kwa mwaka huu wa 2012, ombi lililotolewa kukidhi misaada ya kibinadamu lilifanikiwa kwa asilimia 60 tu na hivyo kudhihirisha kuwa misaada ya kibinadamu haikuwafikia watu wote waliohitaji.