Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNHCR yajiandaa kupeleka misaada Syria iwapo mapigano yatasitishwa

UNHCR yajiandaa kupeleka misaada Syria iwapo mapigano yatasitishwa

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR limejiandaa kupeleka misaada ya dharura kwa maelfu ya familia za raia wa Syria kwenye maeneo yasiyofikika kutokana na mapigano iwapo makubaliano ya kusitisha mapigano hayo kwa siku nne wakati wa sikukuu tukufu ya Eid El Adha yatafikiwa.

Mwakilishi wa UNHCR mjini Damascus, Syria Tarik Kurdi amesema UNHCR na washirika wake wanataka wawe katika mazingira ambayo wataingia haraka katika maeneo hayo iwapo hali ya usalama itaruhusu katika siku chache zijazo.

Misaada hiyo ni kwa ajili ya familia 13,000 zilizopo Aleppo, Homs, Al Ragga na Hassakeh ambapo kila familia itapatiwa kifurushi cha kilo 42 kinachojumuisha vifaa vya nyumbani ikiwemo magodoro manne, mablanketi manne, vifaa vya jikoni, chombo cha kubebea maji na sabuni.

Wito wa kusitisha mapigano wakati wa sikukuu umekuwa unatolewa na Mjumbe wa amani wa Umoja wa Mataifa na Umoja wa nchi za kiarabu kwa Syria, Lakhdar Brahimi.