Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baraza la Usalama lalaani mashambulizi ya kigaidi Aleppo, Syria

Baraza la Usalama lalaani mashambulizi ya kigaidi Aleppo, Syria

Wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, leo wamelaani vikali mashambulizi ya kigaidi ambayo yalitekelezwa siku ya Jumatano katika mji wa Aleppo nchini Syria, ambayo yalisababisha vifo kadhaa na kuwajeruhi mamia ya watu.

Wameelezea huzuni wao na kutoa ujumbe wa rambirambi kwa jamaa za waathiriwa wa vitendo hivyo vya kikatili.  Katika taarifa kwa vyombo vya habari, Baraza hilo limesema kuwa kundi la wanamgambo wa kiislamu la Jebhat al-Nusra, ambalo lina uhusiano na Al-Qaeda, limedai kutekeleza mashambulizi hayo.

Kwa mujibu wa vyombo vya habari, bomu mbili zililipuka ndani ya gari siku ya Jumatano katika eneo la hadharani la Saadallah al-Jabiri katika mji wa Aleppo, na nyingine mwendo usio mbali sana na hapo, na kuwaua watu 48. Wanachama wa Baraza la Usalama wamesema ugaidi wa aina zote unahatarisha kwa kiasi kikubwa amani na usalama duniani, na wamesema wataendelea kujitolea kukabiliana nao, chini ya majukumu yake kulingana na mkataba mkuu wa Umoja wa Mataifa.