Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Miradi inayosaidiwa na Global Fund imeanza kuzaa matunda

Miradi inayosaidiwa na Global Fund imeanza kuzaa matunda

Mfuko wa kimataifa wa kupambana na ukimwi, kifua kikuu na malaria yaani Global Fund Jumatano umetangaza kwamba nchi zinazofaidika na msaada wake zimewaweka watu wengi zaidi katika kupata dawa za kufubaza virusi vya HIV na kuzuia watoto wengi zaidi kuzaliwa wakiwa na virusi hivyo. Mfuko huo unasema haya ni matunda mazuri kuwahi kuonekana licha ya sasa kuwepo na matatizo makubwa ya kiuchumi yanayosababisha msaada kupungua.

Mkurugenzi mkuu wa mfuko huo wa kimataifa Profesa Michel Kazatchkine ametoa wito kwa wahisani kuongeza msaada wa fedha akisema kwamba wakati matokeo yanaonyesha kwamba miradi inayosaidiwa na Global Fund inazaa matunda, matokeo zaidi yanaweza kufikiwa kukiwa na fedha zaidi.

Mamilioni ya watu katika nchi masikini wanategemea mfuko wa kimataifa ili waweze kuendelea kuishi na kuwa na afya ili waweze kuishi maisha ya kawaida.