Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Bodi ya raga yapongezwa kwa kupambana na njaa:UM

Bodi ya raga yapongezwa kwa kupambana na njaa:UM

Bodi ya kimataifa ya mchezo wa raga imepongezwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon kwa jukumu kubwa ililochukua kupambana na njaa duniani.

Katibu Mkuu akizungumza kwenye hafla maalumu katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa hapa New york kwenye uzinduzi wa kombe la dunia la raga kwa 2011 amesema, raga ni mchezo unaochagiza afya, kufanya kazi kwa pamoja na urafiki.

Amesema anaweza kuwa sio mchezaji wa raga lakini ni shabiki mkubwa wa bodi ya kimataifa ya mchezo huo. Amesema bodi hiyo imekuwa ikishirikiana na shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP ili kusaidia kushughulikia matatizo ya njaa duniani.

Ban amesema kwa miaka saba sasa kupitia mpango maalumu Tacle Hunger Programme bodi ya raga imeelimisha na kuchangisha fedha zilizosaidia kuleta mabadiliko makubwa katika maisha ya watu.