Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mashambulio dhidi ya viongozi wa Usomali yalaaniwa na UM

Mashambulio dhidi ya viongozi wa Usomali yalaaniwa na UM

Ahmedou Ould-Abdallah, Mjumbe Maalumu wa KM kwa Usomali, amelaani vikali mashambulio ya karibuni yaliofanyika Mogadishu yaliowalenga wabunge, hujumu ambazo alisema zilikusudiwa hasa kuzorotisha juhudi za Serikali mpya ya Usomali za kupitisha Bungeni kanuni za Sharia, pamoja na kukwamisha zile jitihadi za kurudisha utulivu na amani ya eneo.

Kwenye taarifa iliotolewa kwa waandishi habari, Ould-Abdallah alishtumu mauaji yaliotukia Ijumatano ya Mbunge mmoja wa Usomali, pamoja na shambulio jengine liliotukia Alkhamisi la kujaribu kumwua Mjumbe wa Baraza la Mawaziri. Mashambulio haya mawili yanafuatia tukio la mwisho wa mwezi Machi, ambapo bomu liliotegwa barabarani liliripuka mjini Mogadishu na kumjeruhi Waziri wa Mambo ya Ndani, na wakati huo huo kumwua mmoja wa wasaidizi wake.