MUHTASARI WA HABARI: GAZA, HAITI, SUDAN
MUHTASARI WA HABARI: GAZA, HAITI, SUDAN
Hii leo Muhtasari wa Habari unamulika Gaza, Haiti na Sudan Kusini ambako kote ni majanga juu yamajanga na mwasilishaji wako ni Anold Kayanda
Wakimbizi
Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR), pamoja na wadau wake 123, Alhamis ya leo limetangaza kuwa linatafuta dola bilioni 1.4 mwaka huu ili kukidhi mahitaji ya wakimbizi milioni 2.3 wa Sudan Kusini wanaoishi katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Ethiopia, Kenya, Sudan na Uganda. Janga la wakimbizi wa Sudan Kusini linasalia kuwa ndilo kubwa zaidi barani Afrika.
GAZA
Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi wa kipalestina (UNRWA) leo Machi 28 limetahadharisha kuhusu ujio wa baa la njaa katika Ukanda wa Gaza. UNRWA imesema yenyewe ni uti wa mgongo wa misaada ya kibinadamu Gaza lakini bado misafara yao ya chakula imezuiwa kufika kaskazini, ambako baa la njaa linajongea. Wakati huo huo Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Duniani (WHO) limesema kati ya hospitali 36 katika Ukanda wa Gaza, ni 10 tu ambazo zimesalia zikifanya kazi japo nazo kwa kiasi kidogo.
Haiti
Ripoti ya Ofisi ya Haki za Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa iliyochapishwa leo inataka hatua za haraka na za ujasiri ili kukabiliana na hali ya "janga" nchini Haiti. Ripoti imeeleza kuwa magenge yanaendelea kutumia unyanyasaji wa kingono kuwatendea unyama, kuwaadhibu na kuwadhibiti watu. Wanawake wamebakwa hata baada ya kushuhudia waume zao wakiuawa mbele yao. Magenge pia yanaendelea kuajiri na kunyanyasa watoto wavulana na wasichana ambao hawawezi kutoroka kutokana na kuogopa kuuawa