Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Taasisi ya Elsie yapatia UNFIL fedha kuimarisha usawa wa kijinsia

Timu ya wauguzi wa kikosi cha Indonesia kwenye mpango wa Umoja wa Mataifa UNFIL wakienda kutoa huduma kwenye moja ya nyumba katika Kijiji cha Rabb Tlettine, Kusini mwa Lebanon. (12 Oktoba 2012)
Picha na UNIFIL
Timu ya wauguzi wa kikosi cha Indonesia kwenye mpango wa Umoja wa Mataifa UNFIL wakienda kutoa huduma kwenye moja ya nyumba katika Kijiji cha Rabb Tlettine, Kusini mwa Lebanon. (12 Oktoba 2012)

Taasisi ya Elsie yapatia UNFIL fedha kuimarisha usawa wa kijinsia

Wanawake

Mfuko wa Elsie wa kufadhili wanawake walioko kwenye operesheni za ulinzi wa amani, EIF, hii leo umetangaza mchango wa dola 357,000 kwa ajili ya ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Lebanon, UNFIL. 

Taarifa ya mfuko huo iliyotolewa leo jijini New York, Marekani imesema UNFIL inakuwa ya operesheni ya kwanza ya ulinzi wa amani kupokea fedha hizo ambazo zitatumika kuweka mazingira wezeshi na jumuishi kwa ajili ya walinda amani wanawake. 

Mathalani fedha hizo zitaewezesha UNFIL kujenga mazingira bora ya malazi yanayojali jinsia pamoja na kazi kwa ajili ya wanawake walinda amnai kutoka Ghana ambao wanahudumu kwenye ujumbe huo. Halikadhalika fedha hizo zitawezesha UNFIL kufikia usawa wa jinsia katika uongozi. 

EIF ni taasisi iliyoanzishwa kwa pamoja na Umoja wa Mataifa na Canada mwaka 2019, ambapo Sekretarieti yake iko ndani ya Shirika la Umoja wa Mataifa la kushughulikia masuala ya wanawake UN-Women na inafadhiliwa na nchi wanachama. Hadi sasa jumla ya dola milioni 30 zimeshachangishwa. 

Akizungumzia hatua ya leo, Mkurugenzi Mtendaji wa UN Women Sima Bahous amesema “ili operesheni za ulinzi wa amani zifanikiwe tunahitajika ushiriki wa wanawake walinda amani wengi zaid. Lakini hadi sasa usawa katika operesheni hizo unakwamishwa na mazingira na malazi yasiyojali jinsia.”