Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Omicron isidharauliwe na kukosa usawa wa chanjo kunatuumiza zaidi - WHO

Mwanamke akipimwa Covid-19 katika kliniki huko Palestina
©UNDP/Abed Zagout
Mwanamke akipimwa Covid-19 katika kliniki huko Palestina

Omicron isidharauliwe na kukosa usawa wa chanjo kunatuumiza zaidi - WHO

Afya

“Kutokana na kuenea kwa mnyumbuliko mpya wa omicron katika maeneo yote duniani, maambukizi mapya yalifikia milioni 9.5 na vifo vilizidi 41,000 ulimwenguni kuanzia Desemba 27 hadi Januari 2. "Na tunajua kwamba namba hizi ziko chini ya zile halisi." Anaonya Mkurugenzi Mkuu wa shirika la Afya la Umoja wa Mataifa, Dkt Tedros Ghebreyesus akitoa wito kwa mara nyingine tena kwa usambazaji sawa wa chanjo dhidi ya virusi vya corona. 

Akizungumza hii leo na wanahabari mjini Geneva Uswisi, Dkt Tedros amesema, "upatikanaji usio sawa wa chanjo unaua watu, unagharimu kazi na unadhoofisha ufufuaji wa uchumi wa dunia. Alpha, beta, delta, gamma na omicron zinaonesha kwamba, kwa kiasi fulani kutokana na viwango vya chini vya chanjo, tumeunda hali bora zaidi za kuibuka kwa mnyumbuliko wa virusi. Wiki iliyopita, idadi kubwa zaidi ya mambuki ya COVID-19 ziliripotiwa hadi sasa katika janga hilo.”  

Katika mkutano wake wa kwanza wa mwaka huu wa 2022 wa kuripoti hali ya janga hili, Tedros Adhanom Ghebreyesuss amegusia kwa wasiwasi juu ya ongezeko la asilimia 71 ya maambukizi yalitambuliwa na kusajiliwa kutoka wiki ya Desemba 27, 2021 hadi Januari 2, 2022 wakati, kwa mujibu wa takwimu kutoka kwa WHO, kulikuwa na karibu maambukizi mapya milioni 9.5 na zaidi ya vifo 41,000, licha ya ukweli kwamba vifo vilipungua kwa asilimia 10. 

"Na tunajua kwa kweli kwamba hii ni hesabu ya chini kwa sababu namba zilizoripotiwa hazioneshi mkusanyiko wa ushahidi wakati wa siku za sikukuu, idadi ya vipimo vya nyumbani visivyo na nyaraka na mifumo ya ufuatiliaji iliyozidiwa ambayo hupoteza taarifa za maambukizi ulimwenguni." Ameeleza Dkt. Tedros. 

Takwimu hizo mpya zinaweza kuleta jumla ya maambukizi kufikia Januari 2 hadi milioni 289, wakati vifo vina jumla ya zaidi ya milioni 5.4 ulimwenguni. 

Omicron isidharauliwe 

Mnyumbuliko wa omicron kwa sasa unatawala ueneaji wa virusi vya corona na ingawa unaonekana kuwa si mbaya zaidi kuliko delta, haswa miongoni mwa watu waliochanjwa, Dkt Tedros anaonya kuwa "haifai kuainishwa kama lahaja 'isiyo kali'. " 

"Kama minyumbuliko ilivyotangulia, omicron inalaza hospitalini na kuua watu. Tsunami ya mmambukizi ni kubwa na ya haraka sana hivi kwamba inalemea mifumo ya afya kote ulimwenguni. Hospitali zinakuwa na msongamano wa watu na upungufu wa wafanyakazi, hivyo kusababisha vifo vinavyoweza kuzuilika sio tu kutoka kwa COVID-19, bali pia magonjwa na majeraha mengine ambapo wagonjwa hawawezi kupata huduma kwa wakati.” Bwana Tedros anasisitiza.