Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wahudumu wa kibinadamu ni mashujaa wanaoweka rehani maisha yao ili kuokoa ya wengine:Guterres

Wahudumu wa afya katika kiliniki inayosaidiwa na UN karibu na kambi ya wakimbizi wa ndani ya Ceel Jaale katika eneo la Belet Weyne wakimuhudumia mama na bintiye mdogo.
UNSOM
Wahudumu wa afya katika kiliniki inayosaidiwa na UN karibu na kambi ya wakimbizi wa ndani ya Ceel Jaale katika eneo la Belet Weyne wakimuhudumia mama na bintiye mdogo.

Wahudumu wa kibinadamu ni mashujaa wanaoweka rehani maisha yao ili kuokoa ya wengine:Guterres

Msaada wa Kibinadamu

Ikiwa leo ni siku ya huduma za kibinadamu duniani Umoja wa Mataifa umesema unawaenzi wahudumu hao ambao wanakabiliana na changamoto lukuki katika kuokoa na kuboresha maisha ya mamilioni ya watu. 

Kupitia ujumbe wake maalum wa siku hii Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema “wahudumu hawa ni mashujaa wa kweli na wanafanya maajabu katika nyakati ngumu ili kusaidia wanawake, wanaume na watoto ambao maisha yao yamesambaratishwa na majanga.”

Ameongeza kuwa mwaka huu wahudumu wa kibinadamu wamelemewa kuliko wakati mwingine wowote “Wanakabiliana na janga la kimataifa la COVID-19 ambalo limesababisha ongezeko kubwa la mahitaji ya kibinadamu kutokana na athari zake. Kupoteza ajira, elimu, chakula, maji na usalama vinawasukuma mamilioni ya watu katika hali mbaya.” 

Katibu mkuu amesema vikwazo vya kusafiri ili kupunguza kusambaa kwa maambukizi ya virusi vya corona vinamaanisha kwamba jamii, asasi za kiraia na mashirika ya kijamii kugeuka kuwa wahudumu wa kwanza kuliko ilivyokuwa awali. 

Na kwa mantiki hiyo Guterres amesema “Mwaka huu tunawasherehekea wao, watu ambao mara kwa mara wana mahitaji yao, kama vile wakimbizi kuzisaidia jamii zinazowahifadhi, wahudumu wa afya ambao wanawahudumia wagonjwa na kutoa chanjo kwa watoto na wahudumu wa kibinadamu ambao wanajadili kupata fursa katika maeneo ya vita ili kufikisha chakula, maji na madawa. Ni mashujaa wasiotarajiwa wa kukabiliana na janga hili na mara nyingi wanaweka rehani maisha yao ili kuokoa yaw engine.” 

Katibu Mkuu ametoa wito kwa dunia kuungana naye katika siku hii ili kutoa shukran na msaada kwa wahudumu hao jasiri wa kibinadamu, wahudumu wa afya na wato hudumu ya kwanza ambao wanaonyesha mshikamano na utu katika wakati huu wenye mahitaji makubwa yasiyotarajiwa.