Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mlinda amani wa Umoja wa Mataifa auawa Kivu Kaskazini, UN yalaani vikali

MONUSCO yashiriki kurejesha amani huko Lodja, DRC
MONUSCO
MONUSCO yashiriki kurejesha amani huko Lodja, DRC

Mlinda amani wa Umoja wa Mataifa auawa Kivu Kaskazini, UN yalaani vikali

Amani na Usalama

Mwakilishi maalum wa Umoja wa Mataifa na mkuu wa mpango wa Umoja huo nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo MONUSCO, amelaani vikali mauaji ya mlinda amani wa Umoja wa Mataifa yaliyofanyika usiku wa kuamkia leo.

Katika taarifa ya mwakilishi huyo Leila Zerrougui iliyotolewa leo mjini Kinshasa, mlinda amani huyo kutoka Indonesia ameuawa na wanaoshukiwa kuwa ni wapiganaji wa ADF waliposhambulia walinda amani wa MONUSCO waliokuwa kwenye doria eneo la Makisabo karibu na mji wa Ben , Kivu Kaskazini na mlinda amani mwingine amejeruhiwa katika shambulio hilo.

Bi. Zerrougui ameelezea kusikitishwa kwake na kuendelea kwa vitendo hivyo na pia ametuma salamu za rambirambi kwa familia ya marehemu na serikali ya Indonesia na amemtakia ahuweni ya haraka majeruhi.

Leila Zerrougui, Mwakilishi Maalum na Mkuu wa MONUSCO akihutubia Baraza la Usalama
UN /Loey Felipe
Leila Zerrougui, Mwakilishi Maalum na Mkuu wa MONUSCO akihutubia Baraza la Usalama

 

Waathirika wa shambulio hilo walikuwa wanahusika na ujenzi wa daraja katika kitongoji cha Hululu. Mwakilishi huyo wa Umoja wa Mataifa amesisitiza kuhusu kujitolea kunakofanywa na wanawake na wanaume walinda amani, ambao wanahatarisha maisha yao kila siku wakiwa mbali na nyumbani ili kuwalinda raia na kurejesha amani na utulivu Mashariki mwa DRC.

Ameongeza kuwa mawazo na fikra zake ziko pamoja pia na majeshi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ambayo yanashiriki operesheni kubwa ya kupambana na waasi na kuleta amani, familia zao na raia wote wa DRC ambao ni waathirika wa mashambulizi ya makundi ya waasi na wapiganaji wanaoendelea kuleta machafuko Mashariki mwa nchi hiyo.