Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

IFAD yatoa ombi la msaada kwa ajili ya kuimarisha maisha ya watu vijijini

Mkulima wa ufuta akivuta zao hilo
IFAD
Mkulima wa ufuta akivuta zao hilo

IFAD yatoa ombi la msaada kwa ajili ya kuimarisha maisha ya watu vijijini

Ukuaji wa Kiuchumi

Mfuko wa maendeleo ya kilimo duniani, IFAD unatoa wito kwa nchi wanachama kusaidi kuimarisha juhudi zake maradufu kwa ajili ya maisha ya watu wa jamii zilizotengwa kufikia mwaka 2030.

Akizunugmza katika mkutano huko Roma, Italia, rais wa IFAD Gilbert Houngbo  ametoa pendekezo la prgoramu ya dola bilioni 30 kwa ajili ya kazi katika kipindi cha miaka kumi ijayo ili kukabiliana na changamoto zinazowakabili watu vijijini.

Bwana Houngbo, ameongeza kwamba, “kote ulimwenguni mabadiliko ya tabianchi yanaathiri mifumo ya vyakula. Kina cha bahari cha maji kinaendelea kupanda. Mabadiliko ya tabia nchi yanatokea mara kwa mara na yana athari kubwa. Mazao ya chakula yanatishiwa na ukame, mafuriko na moto. Isitoshe mizozo na udhaifu unaathiri watu wa vijijini na ni watu wa vijijini hususan wakulima wadogowadogo ambao huathirka pakubwa.”

Wito wa leo wa kuimarisha uwekezaji  unaashiria uzinduzi wa IFAD wa mchakato wa mwaka mzima wa mashauriano ambapo nchi wanachama wa IFAD wanakusanyika ili kukubaliana kwa mwelekeo wa kimkakati na kuhamasisha fedha ili kuwezesha IFAD kutoa kama mikopo ya kawaida na misaada kwa nchi zinazoendelea.

Rais huyo wa IFAD amesema, "matarajio yetu ni kuwa na programu ya mikopo na ruzuku kati ya dola bilioni 4 na dola bilioni 5 kwa kipindi cha mwaka 2022 hadi 2025. Sekta thabiti ya kilimo inategemea mfumo endelevu wa chakula. "

Mali, nchi ambayo hivi sasa inakabiliwa na ongezeko la migogoro na ukosefu wa uhakika wa chakula na mabadiliko ya tabianchi, imeshuhudia matokeo ya mipango ya maendeleo ya muda mrefu ya IFAD nchini. AKizungumza kwenye mkutano huo rais wa Mali Ibrahim Boubacar Keïta, amesema, "Mali haitakata tamaa. Sisi wala nchi zingine za Sahel. Tunavuja damu lakini tutashinda kwa msaada wa mashirika kama IFAD. "

Rais huyo wa Mali ameongeza kwamba, "Kile ambacho IFAD imefanya katika nchi yetu, ni mambo ya hali ya juu zaidi na imetuwezesha sisi, watu ambao wanakabiliwa na changamoto mbaya zaidi, ambayo, licha ya yote, kushikilia maadili yetu, na kuweka hadhi yetu."

Kwa kuongeza msaada kutoka kwa nchi wanachama, IFAD inalenga kuimarisha uzalishaji wa takriban wakulima wadogo wadogo milioni 200, kujengea mnepo zaidi ya watu milioni moja vijijini, na kuongeza mapato ya wanawake na wanaume wa vijijini karibu milioni 260 na angalau asilimia ishirini ifikapo mwaka 2030.