Mapinduzi ya kijeshi Mali, UN yazungumza
Mapinduzi ya kijeshi Mali, UN yazungumza
Kufuatia taarifa za mapinduzi ya kijeshi nchini Mali, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametoa taarifa yake akisema kuwa anafuatilia kwa karibu kinachoendelea kwenye taifa hilo la Afrika Magharibi.
Taarifa ya msemaij wake iliyotolewa leo jijini New York, Marekani imesema kuwa “Guterres anafuatilia na wasiwasi mkubwa kile kinachoendelea Mali, ikiwemo kuasi kwa jeshi kulikotamatika kwa kukamatwa kwa Rais Ibrahim Boubacar Keita na viongozi kadhaa wa serikali yake mapema leo.”
Katibu Mkuu amelaani vikali vitendo hivyo na kutaka kurejeshwa haraka kwa utawala wa kikatiba na kisheria nchini Mali.
Amesema “kumaliza hili nasihi kuachiliwa huru bila masharti yoyote kwa Rais Keïta na mawaziri wake.”
Katibu Mkuu amesisitiza wito wake wa mashauriano na suluhu ya amani ili kumaliza tofauti zozote zilizopo.
Ameeleza kuwa anaung amkono juhudi za Muungano wa Afrika na Jumuiya ya uchumi ya nchi za Afrika Magharibi, ECOWAS katika kusaka suluhu ya kudumu na kwa amani nchini Mali ikiwemo kupitia kwa ofisi za mwakilishi wake maalum kwa Afrika Magharibi, UNOWA.
Halikadhalika amesihi wadau wote hususan vikosi vya ulinzi na usalama vijizuie kwa kiasi kikubwa na kuzingatia haki za binadamu na uhuru wa raia wote wa Mali.