Wakimbizi Warundi takribani 600 wamerejea nyumbani kwa hiari kutoka Tanzania
Shirika la la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi duniani UNHCR na wadau kwa kushirikiana na serikali ya Tanzania leo wamewasaidia wakimbizi takribani 600 wa Burundi kurejea nyumbani kama sehemu ya mpango wa wakimbizi kurudi nyumbani kwa hiari.
UNHCR imeitaka serikali ya Tanzania na Burundi kuhakikisha inaheshimu wajibu wao wa kimataifa wakati wa mchakato huo na kutomrejesha mkimbizi au muomba hifadhi yoyote kwa lazima.
“Tunaisihi serikali ya Tanzania na ya Burundi kuheshimu ahadi zao za kutekeleza matakwa ya kimataifa ya kuhakikisha kila mkimbizi anarejea kwa hiari na kuwa hakuna mkimbizi au msaka hifadhi yeyote anayerejeshwa Burundi bila ridhaa yake.” Imesema UNHCR.
Aidha UNHCR imesema japokuwa haihimizi wakimbizi kurejea Burundi, iko tayari kuendelea kuwasaidia wakimbizi ambao wamefanya chaguao kwa hiari yao kurejea nchini mwao na pia itawasaidia katika kuhakikisha wanarejea katika Maisha ya kawaida huko nchini Burundi.
Kwa mujibu wa takwimu za UNHCR, zaidi ya wakimbizi 76,000 wamesaidiwa kurejea nchini Burundi tangu Septemba 2017.