Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Licha ya machafuko UN yataka wapiga kura kuhakikishiwa haki yao Afghanistan

Uchaguzi wa wabunge nchini Afghanistan,20 Oktoba 2018.Bamyan.Wanawake wasimama katika mstari nje ya kituo kimoja wakijitarisha kupiga kura
Photo UNAMA / Abbas Naderi
Uchaguzi wa wabunge nchini Afghanistan,20 Oktoba 2018.Bamyan.Wanawake wasimama katika mstari nje ya kituo kimoja wakijitarisha kupiga kura

Licha ya machafuko UN yataka wapiga kura kuhakikishiwa haki yao Afghanistan

Amani na Usalama

Mpango wa Umoja wa Mataifa nchini Afghanistan UNAMA unasema licha ya uchaguzi wa bunge hii leo kughubikwa na ghasia umetiwa moyo na idadi kubwa ya wananchi waliojitokeza  kutekeleza haki yao ya msingi ya kupiga kura na kutaka hakikisho kwa wote kuweza kupiga kura.

Katika taarifa iliyotolewa na UNAMA mjini Kabul , ujumbe huo umesema k, kwa kuwa uchaguzi huu ndio wa kwanza tangu mwaka wa 2001 kusimamiwa na Wafghanistan wenyewe , ni uchaguzi muhimu sana katika mchakato wa nchi hiyo kuelekea  kujitegemea.

Mpango huo umesema mamilioni ya  wananchi walijitokeza kwa wingi leo na kusubiri kwa muda mrefu katika foleni ili kuweza kupiga kura licha ya machafuko kadhaa yaliyojitokeza na matatizo ya kiufundi, katika tumeya uchaguzi.

Wafanyakazi wa tume huru ya uchaguzi  (IEC) wakifungua masanduku ya kura kwa ajili ya kuhesabu mjini Herat, Afghanistan 18 Septemba 2010
UNAMA
Wafanyakazi wa tume huru ya uchaguzi (IEC) wakifungua masanduku ya kura kwa ajili ya kuhesabu mjini Herat, Afghanistan 18 Septemba 2010

 

Taarifa ya UNAMA imewapongeza wananchi waliopiga kura kwa kutekeleza haki yao ya kiraia na kuwataka wale  wote waliokosa fursa ya kupiga kura kutokana na matatizo ya kiufundi ya tume ya uchaguzi nao wapewe nafasi ya kutimiza haki yao ya msingi kuchagua wawakilishi wao.

Mpango huo pia umesema unatambua hatua za haraka zilizochukuliwa na tume ya uchaguzi ya Afghanistan kuhakikisha kuwa hakuna mtu yeyote aliye na haki ya kupiga kuraatakayekosa fursa hiyo kutokana na matatizo ya kiufundi yaliyojitokeza, pia serikali imesema kwa vituo ambavyo havikuweza kufunguliwa hii leo basi vitafunguliwa kesho ili zoezi hilo liweze kukamilika.

 Na kwa wapiga kura wa Kandahar ambako uchaguzi uliahirishwa kwa sababu za kiusalama, UNAMA imesema watawezeshwa kupiga kura siku ya jumamosi ijayo .

Hata hivyo duru za habari zinasema ghasia zilighubika baadhi ya maeneo ya kupigia kura na kusababisha vifo vya zaidi ya watu 28 na wengine kujeruhiwa.

Uchaguzi wa Bunge nchini Afghanistan, 20 Oktoba 2018, kituo cha upigaji kura cha BAMYAN.
Picha na UNAMA/Abbas Naderi
Uchaguzi wa Bunge nchini Afghanistan, 20 Oktoba 2018, kituo cha upigaji kura cha BAMYAN.

Uchaguzi huu ambao ni muhimu umeshuhudia hatua mbalimbali zikiwemo za kuzuia uibaji wa kura na kuhusisha wachunguzi na wawakili wa wagombea takriban 400,000 ili kuhakikisha uchaguzi huo unakuwa huru na wa haki.

Umoja wa Mataifa umewahimiza wasimamizi wa uchaguzi, vyama vya kisiasa pamoja na wapiga kura kuchangia katika kulinda mchakato wa uchaguzi hususan  wakati wa kukusanya na kuhesabu kura. Na kwa mtu yreyote atakayekuwa na walakini wa uchaguzi basi awasilishe malalamiko yake kwa tume ya uchaguzi na  tume inayoshughulikia malalamiko ya uchaguzi.

Na endapo madai ni ya msingi basi sheria ishike mkondo wake kwa kufanyika kwa uchunguzi na inapohitajika wahusika wawajibishwe.