Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mazao yaliyotelekezwa sasa kugeuka mkombozi wa njaa:FAO 

Chakula cha asili kama quinoa kimekuwepo kwa karne nyingi , lakini limetelekezwa kwa sababu mazao mengine yanayozalishwa kwa wingi na yenye soko yamechukua nafasi katika mfumo wa kilimo
FAO/MINAG/Heinz Plenge
Chakula cha asili kama quinoa kimekuwepo kwa karne nyingi , lakini limetelekezwa kwa sababu mazao mengine yanayozalishwa kwa wingi na yenye soko yamechukua nafasi katika mfumo wa kilimo

Mazao yaliyotelekezwa sasa kugeuka mkombozi wa njaa:FAO 

Tabianchi na mazingira

Katika historia ya mwandamu, kati ya aina 30,000 za mimea , ni aina 6000 hadi 7000 pekee ndizo zimekuwa zikilimwa kwa ajili ya chakula kufikia leo hii , na ni takriban aina 170 tu za mazao ndio zinatumika kwa kiwango kikubwa katika biashara , kwa mujibu wa ripoti ya shirika la chakula na kilimo FAO iliyotolewa juma hili.

Ripoti hiyo ambayo ni mahsusi kwa ajili ya kuichagiza dunia kukumbatia mazao yaliyotelekezwa na yanayoweza kuhimili mabadiliko ya tabia nchi, inasema cha kushangaza zaidi katika aina maelfu ya mimea ni 30 pekee zinazotegemewa kuwapatia wanadamu mahitaji ya kimiwli yanayohitajika kila siku kama nguvu na virutubisho vingine , na zaidi ya asilimia 40 ya nguvu za miwli zinatokana na aina tatu za nafaka ambazo ni mchele, ngano, na mahindi.

Ripoti hiyo ya FAO inasema kuna maelfu ya mazao yametelekezwa au kutotumiwa ipazavyo kwa karne nyingi na kufanya watu sio tu kwamba wanakosa ladha na utamu wa mazao hayo lakini pia virutubisho muhimu vilivyo katika mazao hayo. Imetaja baadhi ya mazao hayo kuwa ni dungusi kakati ( Cactus pear), ndizi nyekundu (Dacca bannanas), maduriani (durian) na quinoa.

Na imeongeza kuwa mara nyingi mazao haya ni ya asili na yanatelekezwa kwa sababu ama yanamea tu katika sehemu ndogo duniani, hayatoi mazao mengi, yana kazi kubwa , yanashambuliwa kirahisi na wadudu au hayajafanyiwa utafiti wa kutosha, hivyo hayajawahi kuingia katika soko la dunia na kufanya watu wengi kutofahamu kama yapo.

Muuzaji wa matunda ya dunriani nchini Indonesia , tuna la duriani limetajwa kuwa chakula muhimu cha asili katika vita dhidi ya njaa
FAO/Oka Ngurah
Muuzaji wa matunda ya dunriani nchini Indonesia , tuna la duriani limetajwa kuwa chakula muhimu cha asili katika vita dhidi ya njaa

 

Sasa FAO imetoa sababu tano muhimu kwa nini dunia iache kuyatelekeza mazao haya:mosi yana virutubisho muhimu kwa afya ya binadamu ikiwemo vitanini A, B12, D, madini ya chuma, zinc na madini joto , mfano quina ni zao pekee lenye vitu vyote vinavyohitajika katika mwili wa binadamu.

Pili yanapanua wigo na kulinda kilimo na kufanya mifumo ya uzalishaji wa chakula kuwa endelevu na kusaidia kudhibiti wadudu na magonjwa ya mimea. Tatu yanahimili mabadiliko ya tabia nchi , ikiwemo mafuriko na ukame mfano dungusi kakati ambalo huzaa matunda hata kwenye maeneo ya jangwa, nne yanaendeleza elimu ya asili , kwani kwa kuyatelekeza mazao hayo asili ni kutekeleza pia mifumo ya asili kilimo na uvunaji mazao ikiwemo kilimo cha matuta, yanahifadhi maji, hayahitaji mbolea na yanarutubisha udongo. Na tano yanaweza kuwaoko wakulima wadogowadogo na wazalishaji wa asili kwani yanauwezekano mkubwa wa kupata soko la kimataifa kwa ajili ya biashara mfano quinoa zao lililojulikana Zaidi Bolivia, Peru na Equado hadi 2010, lakini sasa linalimwa katika nchi Zaidi ya 70 duniani.