Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ushirikiano wa kimataifa unahitajika kuhakikisha uhakika na usalama wa chakula:UN/AU

Chakula chenye virutubisho vya kutosha vya lishe kinaweza kumwondoa mtu hususani watoto katika hatari ya kupata magonjwa.
World Bank/Maria Fleischmann
Chakula chenye virutubisho vya kutosha vya lishe kinaweza kumwondoa mtu hususani watoto katika hatari ya kupata magonjwa.

Ushirikiano wa kimataifa unahitajika kuhakikisha uhakika na usalama wa chakula:UN/AU

Malengo ya Maendeleo Endelevu

Wanasayansi, watunga sera , wawakilishi wa serikali , wakulima na walaji wanakutana kwa siku mbili mjini Adis Abba Ethiopia kwenye mkutano wa kwanza kuhusu uhakika na usalama wa chakula na jukumu lake katika maendeleo endelevu, SDG’s.

Chakula kisichofaa kilicho na bakteria, virusi, wadudu, na sumu au kemikali husababisha maradhi kwa watu zaidi ya milioni 600  na vifo kwa wengine 42,000 kila mwaka. Na magonjwa yatokanayo na kula chakula kisichofaa huibebesha mzingo mtubwa sekta za afya na kuzorotesha uchumi , biashara na utalii.

Na kwa mujibu wa mashirika ya Umoja wa Mataifa lile la chakula na kilimo FAO, la afya duniani WHO, la kimataifa la utalii WTO na muungano wa Afrika AU ambao ndio waandalizi wakuu wa mkutano huo, gharama za chakula kisichofaa kwa nchi za kipato cha chini na cha wastani ni takribani dola bilioni 95 zinazopotea kila mwaka.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo mkurugenzi wa FAO Grzaziano Da Silva amesema  “Hakuna uhakika wa chakula bila usalama wa chakula, mkutano huu ni fursa nzuri kwa jumuiya ya kimataifa kuimarisha ahadi za kisiasa na kuchukua hatua muafaka. Kulinda chakula chetu ni wajibu wetu wa pamoja , ni lazima wote tushiriki, ni lazima tufanye kazi pamoja kupigia upatu usalama wa chakula katika ajenda za kitaifa na kimataifa.” Lakini nini chanzo cha kutokuwa na chakula salama? David Massey ni mtaalam wa mawasiliano wa FAO

(SAUTI YA DAVID MASSEY)

“Mabadiliko ya tabia nchi, ukuaji wa miji , na kitu cha pili ni mfumo wa kimataifa wa usambazaji chakula, wapi chakula chetu kinakotoka, na tayari kuna chakula kingi kinachonunuliwa kwenye mitandao, nani anayekidhibiti chakula hicho na aina gani ya teknolojia tunayohitaji ili kuhakikisha kwamba chakula hicho ni salama.”

Mtafiti akizipima nyanya katika maabara ya chakula na mazingira ya IAEA huko Seibersdorf, Austria.
IAEA
Mtafiti akizipima nyanya katika maabara ya chakula na mazingira ya IAEA huko Seibersdorf, Austria.

Kwa upande wake mkurugenzi mkuu wa WHO Dkt. Tedros Gebreyesus amesema “Chakula kinapaswa kuwa chanzo la lishe bora sio chanzo cha maradhi au kifo, chakula kisicho salama kimekuwa chanzo cha vifo kwa maelfu ya watu kila mwaka na suala hilo alijapewa uzito unaostahili.”

Naye mwenyekiti wa tume ya Muungano wa Afrika Moussa Faki Mahamat akiunga mkono hoja hizo amesema “Mkutano huu wa uhakika na usalama wa chakula ni dhihirisho la ushirika wetu, kwani bila chakula salama hatuwezi kufikia lengo la uhakika wa chakula.”

Mkutano huo wa kimataifa utakaomalizika kesho umewaleta pamoja wadau kutoka nchi 130 duniani ili kujadili njia bora za kuhakikisha uhakika na usalama wa chakula.