Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wafasiri wa lugha wana nafasi kubwa katika kufanikisha amani na maelewano duniani

Lydie Mpambara (kushoto) wa Idara ya Baraza Kuu na mikutano ya Umoja wa Mataifa akihojiwa na Anold Kayanda wa UN News Kiswahili
UN News/Assumpta Massoi
Lydie Mpambara (kushoto) wa Idara ya Baraza Kuu na mikutano ya Umoja wa Mataifa akihojiwa na Anold Kayanda wa UN News Kiswahili

Wafasiri wa lugha wana nafasi kubwa katika kufanikisha amani na maelewano duniani

Masuala ya UM

Siku ya kimataifa ya tafsiri  ya lugha imefanyika ulimwenguni huku suala la nafasi ya tafsiri kwenye kuendeleza amani, biashara na maelewano ya kijamii likipigiwa chepuo. Je katika Umoja wa Mataifa tafsiri ya lugha ina faida gani?

Tafsiri kutoka lugha moja  hadi nyingine imekuwa ina mchango mkubwa katika utekelezaji wa majukumu ya Umoja wa Mataifa, amesema Lydie Mpambara, mmoja wa wafasiri wa lugha kwenye idara ya Baraza Kuu na mikutano  ya Umoja huo, DGACM.

Akihojiwa na Idhaa ya Kiswahili ikiwa sehemu ya maadhimisho ya siku ya tafsiri ya lugha duniani iliyoadhimishwa hivi karibuni, Bi. Mpambara ambaye anazungumza kiingereza, kifaransa, Kiswahili na kispanyola amefafanua jinsi kazi yao inavyochagiza majukumu ya Umoja wa Mataifa. 

Kazi yetu haionekani mtu hajui tunafanya nini, lakini watu hawawezi kuelewana iwapo hawazungumzi lugha moja. Sasa tunafanya lugha hizo zinakuwa lugha moja

Amesema "tafsiri kwa Umoja wa Mataifa ni kitu muhimu sana kwa sababu unaona kuna nchi nyingi  sana watu wanatakiwa waelewane, sasa kama kila mtu ana lugha yake, tafsiri inafanya watu waelewane halafu wakubaliane. Mfano sasa Afrika au mahalikuna watu wanalinda amani watafsiri wanafanya kazi muhimu sana. Kama Congo, watu wanaongea Kiswahili au lugha nyingine za Congo. Kuna wakalimani wapo hapo vijijini wanasaidia, labda mtu anatoka Australia atakubaliana vipi na  mtu wa Congo? Kazi yetu haionekani mtu hajui tunafanya nini, lakini watu hawawezi kuelewana iwapo hawazungumzi lugha moja. Sasa tunafanya lugha hizo zinakuwa lugha moja." 

Bi. Mpambara akaulizwa iwapo maendeleo ya teknolojia hususan kwenye fani ya tafsiri yanatishia utekelezaji wa majukumu yao ambapo amesema. "hapana hiyo ni kusaidia tu kwa sababu Google Translate ni kitu kizuri sana,  kinafanya kazi vizuri unaweza kuweka sentensi ukaona inatafsiri hivyo hivyo. Lakini inatafsiri kitu kama kifupi. Lakini kama unatafsiri kitu kirefu inatakiwa uelewe mantiki inayoendana na hicho kitu, mfano kama sheria, Google itatafsiri kama mtu anaongea. Kwa hiyo kazi haiwezi kupotea kwa sababu kuna kitu cha kibinadamu ambacho hizo roboti au programu haziwezi kufanya."