Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Tushirikiane tulinde  lugha za asili- Guterres

Mwakilishi wa jamii ya watu wa asili akihutubia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa
UN/Eskinder Debebe
Mwakilishi wa jamii ya watu wa asili akihutubia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa

Tushirikiane tulinde  lugha za asili- Guterres

Utamaduni na Elimu

Lugha za asili zikiwa hatarini kutoweka, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametaka hatua zaidi kulinda lugha hizo na haki nyinginezo za kundi hilo. Jason Nyakundi na taarifa zaidi.

Kauli hiyo ya Guterres imo kwenye ujumbe wake wa siku ya kimataifa ya lugha za asili inayoadhimishwa tarehe 9 Agosti kila mwaka, ambapo maadhimisho yanaenda sambamba na mwaka 2019 ambao ni mwaka wa kimataifa wa lugha za asili ikilenga kusaka hatua za haraka kulinda, kuchagiza na kuendeleza lugha za asili.

Guterres amesema lugha ni jinsi ambavyo watu wanawasiliana, na lugha ina uhusiano na tamaduni, historian a utambulisho.

Hata hivyo amesema licha ya umuhimu huo, nusu ya takribani lugha 6,700, idadi kubwa ikiwa ni zile za asili, ziko hatarini kutoweka.

Katibu Mkuu ameesema, kwa kila lugha inayotoweka, dunia inapoteza utajiri wa tamaduni na ufahamu.

Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa hivi sasa kuna watu milioni 370 wa jamii za asili ambao Guterres amesema, “idadi kubwa wanakosa haki zao za msingi, huku mifumo iliyowekwa ya kibaguzi na uenguaji ikiendelea kutishia mbinu zao za maisha, tamaduni  na utambulisho wao.”

Katibu Mkuu amesema hali hiyo ni kinyume kabisa na azimio la Umoja wa Mataifa la haki za watu wa asili pamoja na ajenda 2030 ya maendeleo endelevu ambayo ina ahadi ya kutomwacha nyuma mtu yeyote.

Kwa mantiki hiyo Katibu Mkuu amesema ni matumaini  yake kuwa nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa zitashirikiana kikamilifu kuhakikisha watu wa asili wanashikiri katika kupanga maendeleo yao kupitia sera shirikishi, za usawa na zinazotekelezeka.

Amesema Umoja wa Mataifa kwa upande wake uko tayari kusaidia mipango inayolenga kufanikisha upatikanaji wa haki za watu wa asili.