Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UN yalaani mauaji ya raia 200 yaliyofanywa na ISIL Syria

Familia ambazo zimekimbia mapigano kati ya ISF na ISIL magharibi mwa Mosul, Iraq
UNICEF/Romenzi
Familia ambazo zimekimbia mapigano kati ya ISF na ISIL magharibi mwa Mosul, Iraq

UN yalaani mauaji ya raia 200 yaliyofanywa na ISIL Syria

Haki za binadamu

Umoja wa Mataifa  umelaani shambulio la kutisha lililofanywa na magaidi wa ISIL kwenye maeneo yanayokaliwa na raia wengi huko jimbo la As-Sweida kusini-magharibi mwa Syria.

Msemaji wa ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa Ravina Shamdasani amesema hayo leo huko Geneva, Uswisi akizungumza nawaandishi habari akieleza kuwa wamepokea ripoti ya kwamba zaidi ya watu 200 waliuawa kwenye mashambulio lukuki.

Akifafanua zaidi kuhusu mashambulio hayo Bi. Shamdasani amesema, “wapiganaji kadhaa wa ISIL walivamia nyumba  katika vijiji takriban vinane kwenye maeneo ya vijijini ya mashariki na kaskazini mwa  As-Sweida mashambani, wakiwauwa raia kwa kuwapiga risasi ndani ya nyumba zao na kuwachukua mateka wanawake na watoto. Tumepokea majina  27 ya wanawake na watoto ambao wanaripotiwa  kuchukuliwa mateka kutoka kijiji cha Al-Shbiki mashariki mwa As-Sweida vijijini, ingawa  tunaamini idadi kamili inaweza kuwa kubwa zaidi ya hiyo.”

 Amesema picha ya baadhi ya wanawake hao mateka baadaye zilichapishwa katika mtandao wa Twitter zikiambatana na vitisho kuwawatachomwa moto wakiwa hai iwapo serikali haitakomesha harakati zake za kijeshi dhidi ya wapiganaji wa ISIL katika maeneo ya magharibi mwa jimbo la Daraa na pia kuwaachilia huru wanawake na wanaume wa ISIL wanaoshkiliwa na serikali.

Bi. Shamdasan amesema wanaelewa kuwa  wanamgambo wa ISIL wengi wao ni wale walioondolewa na kuhamishwa kutoka kambi ya wakimbizi wa kipalestina ya Yarmouk,  Hajar Al-Aswadna Al-Tadamon kusini mwa Damascus kama sehemu ya mpango wa serikali  wa makubaliano ya usuluhishi.

Imeripotiwa kuwa serikali inatumia makubaliano ya aina hiyo kwenye maeneo ambako inakaribia kuyatwaa ili kuyapatia makundi yaliyojihami uamuzi wa kuridhiana na serikali au kuhamishiwa maeneo ambako hayashikiliwa na serikali.

Amesema hatua ya kuhamisha wapiganaji inaweza kuleta hatari zaidi ya mashmbulizi kwa raia.

Kwa mantiki hiyo ameitaka serikali ya Syria kuwajibika  kuchukua hatua  kuzuia vitendo ambavyo vinaweza  kuhatarisha maisha ya raia wa kawaida pamoja na kutoyaweka makundi yenye silaha  kama vile ISIL katikati mwa raia.

Halikadhalika amesema serikali ya Syria ni lazima ihakikishe kuwa  wale wote wanaotenda makosa ya jinai na wanaokiuka haki za binadamu wanawajibishwa  kwa mujibu wa sheria  na viwango vya sheria za kimataifa.

 

 

Tweet URL