Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Tuna hofu na kinachoendelea Saudi Arabia dhidi ya watetezi wa haki- UN

bendera ya Saudi Arabia ikipepea makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, New York
UN Photo/Loey Felipe
bendera ya Saudi Arabia ikipepea makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, New York

Tuna hofu na kinachoendelea Saudi Arabia dhidi ya watetezi wa haki- UN

Haki za binadamu

Umoja wa Mataifa una wasiwasi kutokana na visa vinavyoendelea nchini Saudi Arabia vya kuwakamata kiholela watetezi wa haki za binadamu pamoja na wanaharakati nchini humo ikiwemo wale wanaotetea haki za wanawake.

Wasiwasi huo umeelezwa na msemaji wa ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa Ravina Shamdasani akizungumza na waandishi habari leo mjini Geneva Uswisi.

Bi. Shamdasani amesema,“tangu tarehe 15 Mei, takriban watu 15 ambao wanaikosoa serikali wamekamatwa na tunaelewa kuwa  wanane kati yao baadaye waliachiliwa huru kwa muda  hadi kukamilishwa kwa kile kilichoitwa mapitio ya taratibu za kesi zao. Baadhi hawajulikani waliko na hakuna uwazi katika utaratibu wakushughulikia kesi zao.”

Ameongeza kuwa ingawa wahusika serikalini wametoa matangazo kuhusu uwezekano wa mashtaka makali dhidi yao , ambapo hukumu inaweza kuwa ya kuwafunga jela kwa kipindi cha miaka 20, bado haijaeleweka ikiwa mashtaka yamewekwa bayana katika kesi hizo zote.

Bi. Shamdasani ameihimiza serikali ya Saudi Arabia iwaachilie huru mara moja bila ya masharti yoyote  wanaharakati wote na watetezi wa haki za binadamu ambao wamekamatwa  kwa sababu za kazi zao  ambazo wamekuwa wakifanya kwa njia za amani pamoja na kampeni ya muda mrefu iliyowezesha kuondolewa  kwa marufuku ya wanawake kuendesha magari.

Msemaji huyo ameongeza kuwa uchunguzi wowote ule ni sharti ufanywe katika njia za wazi ambazo zinaheshimu haki zote na kwamba watetezi wa haki za binadamu na wanaharakati wanapaswa  kuenedelea na kazi zao muhimu za haki za binadamu bila hofu yoyote ya kushtakiwa.

 

Tags: Saudi Arabia,UN, Ravina Shamdasani,