Miji yakua kwa kasi huku mamlaka zimelala- Ripoti
Mamlaka za mikoa na za kitaifa haziendi sawia kuelekea kufanikisha lengo namba 11 la malengo ya maendeleo endelevu, SDGs la kuhakikisha miji inakuwa salama na endelevu ifikapo mwaka wa 2030.
Hivyo ndivyo inakamilisha ripoti mpya ya shirika la makazi la Umoja wa Mataifa la UN-Habitat na washirika wake ambao wanafuatilia maendeleo yaliyofikiwa na changamoto tangu tangu malengo hayo yapitishwe mnamo mwaka wa 2015.
Ripoti hii inakuja sambamba na mkutano wa kwanza wa jukwaa la ngazi ya juu la kisiasa kuhusu SDGs HLPF, ukidurusu malengo sita ikiwemo lengo namba 11 katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa mjini New York nchini Marekani.
Mkurugenzi Mtendaji wa UN-Habitat, Maimunah Mohd Sharif, akihutubia mkutano huo amesema ukuaji wa miji ni moja wa masuala muhimu linapokuja suala la maendeleo endelevu.
(SAUTI YA MAIMUNAH SHARIF)
“Ukuaji wa miji ni nguvu za mabadiliko na pia kuwa chombo cha kuleta suhisho la changamoto za ukuaji wa miji, ikiwa tuna mfumo kama vile utawala bora, uwepo wa miundombinu ya serikali ambao uko tayari kutekeleza lengo namba 11 la maendeleo endelevu.”
Ameongeza kuwa ni lazima wafanye kama inavyohitajika ikiwa wanataka kufanikisha SDGs na pia kuona kama umaskini unatokomezwa, ulinzi wa dunia uimarishwe na kila mmoja anafurahia amani na maendeleo.
Mnamo mwaka wa 2015 nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa, walipitisha SDGs ikiwemo lengo namba namba 11, ikiwa ndio mara ya kwanza miji pamoja mamlaka ya miji kupewa lengo .
Malengo mengine ambayo yana uhusiano na ukuaji wa miji ni maji na kujifasi, nishati endelevu, mazingira pamoja na matumizi endelevu.
Hata hivyo ukuaji wa miji una changamoto zake kadhaa lakini mkuu wa UN- Habitat anataja mbili tu.
(SAUTI YA MAIMUNAH SHARIF)
“Moja, upatikanaji wa nyumba na namba mbili miji inapanuka . Miji inazidi kupanuka na hivyo kumeza maeneo mengi ya ardhi dhidi ya ongezeko la watu.”
Nayo ripoti inasema kuwa ongezeko la watu ikilinganishwa na idadi ya waishio katika sehemu za mabanda na makazi ya kawaida imeongezeka kutoka milioni 807 mwaka wa 2000 hadi milioni 883 mwaka 2014.
Halikadhalika miji inakua kwa kasi kuliko idadi ya watu na hivyo kusababisha kupanda kwa gharama ya miundombinu na ongezeko la magari.