Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Uvumbuzi na ubunifu ni muarubaini kuhakikisha miji endelevu-UN-HABITAT

Kubadilisha dunia: Uvumbuzi kwa ajili ya maisha bora kwa vizazi vijavyo, kauli mbiu mwaka 2019
© UNESCO
Kubadilisha dunia: Uvumbuzi kwa ajili ya maisha bora kwa vizazi vijavyo, kauli mbiu mwaka 2019

Uvumbuzi na ubunifu ni muarubaini kuhakikisha miji endelevu-UN-HABITAT

Malengo ya Maendeleo Endelevu

Zaidi ya nusu ya idadi ya watu duniani hivi sasa wanaishi mijini na kufikia mwaka 2050 theluthi mbili ya watu watakuwa wanaishi mjini na makazi ya kuendana na ongezeko la watu bado hayajakarabatiwa na miji mipya itahitaji kujengwa.

Hiyo ni sehemu ya ujumbe wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres katika maadhimisho ya siku ya miji duniani ambayo haudhimishwa tarehe 31 Oktoba ya kila mwaka ,  mwaka huu ikibeba kauli mbiu, “kubadili dunia: uvumbuzi kwa ajili ya maisha bora kwa vizazi vijavyo.

Katibu Mkuu amesema hali ya sasa na inayotarajiwa inazua fursa nyingi za kubuni na kutekeleza suluhu ambazo zinaweza kukabiliana na janga la mabadiliko ya tabianchi na kuweka njia kwa ajili ya mustakabali endelevu.

Guterres ameongeza kwamba, “miji inatumia theluthi mbili ya kawi au nishati ya umeme ya dunia na inazalisha asimia 70 ya hewa chafuzi. Kimataifa, uamuzi utakaofanyika katika miundombinu mijini katika miongo ijayo kuhusu mipango miji, matumizi bora ya kawi, uzalishaji umeme na usafiri vitakuwa na athau kwa hali ya uchafuzi, kwa kweli ni katika miji ambako vita dhidi ya mabadiliko ya tabianchi kutaibuka ushindi au kupoteza.”

 Hata hivyo Bwana Guterres amesema, licha ya uchafuzi unaotokea mijini lakini miji inachangia asilimia 80 ya pato la taifa kama vituo vya elimu na ujasiriamali, ni kitovu cha uvumbuzi na ubunifu huku vijana wakichukua uongozi.

Kauli hi inaungwa mkono na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la makazi la Umoja wa Mataifa, UN-Habitat Maimunah Mohd Sharif katika ujumbe wake kuadhimisha siku hii amesema changamoto kubwa za dunia sasa kutokana na mabadiliko ya tabianchi ni ukosefu wa usawa, uhamiaji kuelekea mitaa duni huku athari mbaya zikiathiri idadi kubwa ya watu mijini. Kwa mantiki hiyo amesema

(Sauti ya Maimunah)

“Bila mawazo bunifu tutashuhudia ongezeko la joto, malundo ya taka. ongezeko la makazi yasiyo rasmi, ongezeko la msongamano wa magari na kuibuka kwa miji bila mipango, hii ni tofauti na miji jumuishi, salama, endelevu na stahimilivu tunayolenga kuunda kufikia mwaka 2030 kuendana na lengo 11 la malengo ya maendeleo endelevu ya Umoja wa Mataifa, SDGs.”

Bi.Sharif ametoa wito wa kufanya kazi pamoja kuvumbua kwa ajili ya kuleta mabadiliko kote ulimwenguni leo kuhakikisha hakuna atakaye au sehemu itakayowachwa nyuma, akiongeza, “hebu tufanye hilo kwa ajili ya vizazi vijavyo ili warithi dunia bora kuliko ile tulipata kutoka kwa waliotutangulia.”