Afya kwa wote bado kizungumkuti
Unganeni nami kutoa wito wa kila mtu apate huduma ya afya! Ndivyo anavyohitimisha Antonio Guterres, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwenye ujumbe wake wa siku ya afya duniani hii leo.
Bwana Guterres anasema WHO ambalo ni shirika la afya ulimwenguni lilianzishwa miaka 70 iliyopita kwa msingi kwamba kupata huduma bora ya afya ni haki ya kila mtu.
Ingawa hivyo anasema hadi leo hii bado watu wanakosa huduma muhimu za afya licha ya kauli mbiu ya afya kwa wote, UHC.
Anasema ni wazi kuwa magonjwa hatari kama vile ndui yametokomezwa na sasa dunia iko kwenye mwelekeo wa kutokomeza polio, ni vyema kuhakikisha kuwa huduma za msingi za afya zinapatikana kwa kila mtu.
Kwa mantiki hiyo Bwana Guterres anasihi kila mtu aungane na WHO katika kuazimia upya kuhakikisha kila mtu popote pale alipo anapata huduma ya afya anayohitaji.