Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Licha ya mzozo, DRC yakirimu wakimbizi- UNHCR

WFP wagawa msaada Kasai, DRC. Picha: WFP

Licha ya mzozo, DRC yakirimu wakimbizi- UNHCR

Wahamiaji na Wakimbizi

Umoja wa Mataifa umejionea miradi dhahiri ya kilimo, ufugaji na biashara inayotekelezwa huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kwa ajili ya kuwajengea uwezo wakimbizi wanaotoka nchi jirani.

Filippo Grandi ambaye ni Kamishna Mkuu wa wakimbizi kwenye Umoja wa Mataifa ameshuhudia hayo huko Kinshasa, DRC wakati wa ziara yake ya siku nne anayohitimisha leo.

(Sauti ya Filippo Grandi)

“Nimetembelea mradi ulioanzishwa hapa Kinshasa na shirika la SSV kwa lengo la kusaidia wakimbizi. Kuna wakimbizi 800 pekee hapa Kinshasa kutoka nchi jirani na hapa wanawahamasisha kujiongeza na kujiwezesha. Wameanzisha biashara ndogo na masoko na mikakati ambayo inawawezesha kujisaidia.”

Grandi ambaye anaongoza shirika la kuhudumai wakimbizi duniani, UNHCR akazungumzia umuhimu wa hatua hii.

(Sauti ya Filippo Grandi)

“Miradi hii ni ishara pia ya jitihada za nchi hii ya kusaidia wakimbizi kwa kuwapatia fursa za kuweza katika kipindi ambacho wanahitaji kujikwamua na kwa kuwa hawawezi kurejea makwao.”