Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

2017 mwaka mbaya wa kimajanga na athari kwa uchumi: WMO

Mafuriko yanayochangiwa na mabadiliko ya tabianchi. Picha: WMO

2017 mwaka mbaya wa kimajanga na athari kwa uchumi: WMO

Tabianchi na mazingira

Ukame huko Afrika Mashariki, mafuriko makubwa wakati wa pepo za monsuni huko bara ya hindi ni baadhi ya mambo yaliyosababisha mwaka 2017 kuwa mwaka ulioghubikwa na matukio mabaya zaidi ya hali ya hewa. 

Shirika la hali ya hewa duniani WMO limesema hayo hii leo katika ripoti yake iliyotolewa katika siku ya kimataifa ya hali ya hewa, maudhui yakiwa kujiandaa kukabili hali ya hewa na kutumia maji kwa ufanisi.

Ripoti inasema matukio ya hali ya hewa kwa mwaka 2017 yameathiri maendeleo ya kiuchumi, uhakika wa chakula, masuala ya kiafya na pia uhamiaji.

Katibu Mkuu wa WMO Petteri Taalas amesema viwango vya joto kwenye eneo la ncha ya kaskazini mwa dunia vilikuwa ni vya  juu kuliko kawaida huku maeneo yenye watu wengi maeneo ya kaskaizni mwa dunia yakigubikwa na baridi kali pamoja vimbunga vikali vya theluji.

Kenya na Somalia ziliendelea kukumbwa na ukame huku mji wa Cape town nchini Afrika kusini ulikabiliwa na uhaba wa maji.

Ripoti yenyewe  inahakikisha kuwa mwaka wa 2017 umekuwa mmoja wa miaka mitatu ambayo imekuwa yenye joto kali mfululizo na hali hiyo ya joto haikusababishwa na mkondo joto wa bahari au El Nino.

Pia imegusia viashiria vingine  vya tabianchi kama vile kuongezeka kwa mkusanyiko wa hewa ya ukaa, kuongezeka kwa usawa wa baharí, kuyeyuka kwa barafu zilizoko baharini, joto la baharí pamoja na mengine.

Ripoti imeonyesha kuwa hali ya hewa duniani  katika mwaka wa 2017 ilikuwa ya wastani wa nyuzi joto 1.1 katika kipimo cha selsiyasi juu ya vipimo vya wakati wa kabla ya viwanda .