Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watu wengi CAR wanataka kusaka amani na haki- Profesa Knuckey

Watu wengi CAR wanataka kusaka amani na haki- Profesa Knuckey

Kufuatia miaka miaka mingi ya machafuko na vita , kuna watu wengi nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati wanaotaka kusaka amani na haki .

Hayo ni kwa mujibu wa Profesa Sarah Knuckey, mkurugenzi wa kituo cha haki za binadamu  kwenye chuo kikuu cha Columbia mjini New York, Marekani.

Amezuru CAR kwa wiki mbili akiwa pamoja na timu ya wanasheria, wanafunzi na wanasayansi wa uchunguzi wa mauaji, ili kusaidia miradi ya amani na haki.

Timu hiyo imetoa msaada na ushauri wa kitaalamu kwa vyombo vya serikali, mashirika yasiyo ya kiserikali yaani NGO’s na makundi ya asasi za kiraia.

Baraza la usalama la Umoja wa mataifa hivi karibuni limeongeza muda wa mpango wake nchini humo MINUSCAR na kuitaka serikali ya CAR kuendesha maridhiano yanayojumuisha wote baada ya miaka ya vita.

Akiwa CAR Profesa  Knuckey,  amezungumza na mwandishi wa Umoja wa Mataifa, Jean Pierre Ramazani  na kuanza kueleza kikubwa walilochokifanya mjini Bangui

(SAUTI BI KNUCKEY)

Baada ya machafuko mara nyingi tunaona maiti kwenye makaburi ya pamoja zimezikwa kiholela, na familia hazijui nani amezikwa kwenye makaburi hayo na hawana fursa ya kupata haki, timu ya wachunguzi wa mauaji inachoweza kufanya ni kuzisaidia familia kubaini nani amezikwa kwenye makaburi, ili wazikwe kwa heshima huku wakijulikana nani ni nani na pia ushahidi unaweza kukusanywa kubaini sababu ya kifo”