Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Haiti yajitayarisha kwa uchaguzi wa jumapili: UN yatoa wito kwa utulivu

Haiti yajitayarisha kwa uchaguzi wa jumapili: UN yatoa wito kwa utulivu

Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Haiti, MINUSTAH, Sandra Honoré amewaomba raia wa Haiti washiriki kwenye uchaguzi mkuu wa jumapili ijayo na amani na utulivu.

Kwenye taarifa iliyotolewa na Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini humo, Bi Honoré amelezea kutiwa moyo na maandalizi yaliyofanywa kabla ya uchaguzi wa rais, wa serikali za mitaa na raundi ya pili ya uchaguzi wa wabunge unaotakiwa kufanyika jumapili hii, tarehe 25, Oktoba.

Aidha amefuraishwa na jitihada za polisi ya Haiti katika kuhakikisha usalama wa uchaguzi kwa ushirikiano na MINUSTAH.

Amesisitiza kwamba uchaguzi huru, sawa na jumuishi ni lazima ili Haiti iendelee kukuza demokrasia, utawala bora na maendeleo ya jamii.

Awamu ya kwanza ya uchaguzi wa bunge imefanyika tarehe Tisa Agosti, baada ya bunge la Haiti kushindwa kufanya kazi tangu Januari mwaka huu.