Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Dola Milioni 105 zachangishwa kusaidia Somalia

Dola Milioni 105 zachangishwa kusaidia Somalia

Wawakilishi kutoka nchi zaidi ya 40 na mashirika wameahidi dola Milioni 105 kwa ajili ya kusaidia wakimbizi wa Somalia walioko Kenya ili waweze kurejea nyumbani kwa hiari.

Taarifa ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR imesema mchango huo umetangazwa mwishoni mwa mkutano uliofanyika Brussels, Ubelgiji kuchangisha fedha hizo zitakazotumika kutekeleza mpango ulioandaliwa na Somalia kuboresha mazingira ya wanaorejea nyumbani.

Mwenyeji wa mkutano huo ulikuwa ni Tume ya Ulaya kwa kushirikiana na UNHCR ambapo Tume hiyo imeahidi zaidi ya dola Milioni 68 na kati ya hizo Milioni 56 ni kwa ajili ya kusaidia wakimbizi waliorejea Somalia ili wapate huduma za msingi na kuinua vipato vyao.

Halikadhalika usaidizi huo unalenga kuwapatia fursa za ajira wakimbizi elfu 10 waliorejea Somalia.

Mpango huo wa miaka miwili unahitaji dola Milioni 500.