Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Utawala bora suluhu ya kumaliza ugaidi, vijana nao wasipuuzwe: Ban

Utawala bora suluhu ya kumaliza ugaidi, vijana nao wasipuuzwe: Ban

Matarajio ya vijana hususan kwenye nchi ambazo idadi yao ni kubwa yanapaswa kupatiwa kipaumbele na serikali zao, amesema katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon wakati wa kikao cha nchi Saba zilizoendelea kiuchumi zaidi duniani, G7 kinachofanyika huko Ujerumani.Taarifa kamili na Grace Kaneiya.

(Taarifa ya Grace)

Kikao hicho kuhusu ugaidi kinajadili mbinu za kukabiliana na ongezeko la misimamo mikali inayoibua ghasia na vita ambapo Ban amesema vijana ambao hawana mwelekeo wako hatarini zaidi kutumbukizwa kwenye misimamo mikali na ghasia.

Amesema idadi kubwa ya wapiganaji mamluki ni vijana wa kiume wenye umri kati ya miaka 15 na 35 akisema wakishirikishwa katika kuinua maisha yao, wao ndio suluhisho la kumaliza misimamo hiyo hivyo kazi ifanyike kuwashirikisha.

Katibu Mkuu amewaeleza viongozi hao wa G7 kuwa makombora yanaweza kuua magaidi lakini anashawishika kusema kuwa utawala bora ndio unaoua ugaidi hivyo amesihi jamii ya kimataifa kushirikiana kudhibiti ugaidi ikiwemo harakati zinazofadhili vitendo hivyo.