Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Akiwa Washington DC, Ban akutana na viongozi mbali mbali

Akiwa Washington DC, Ban akutana na viongozi mbali mbali

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon aliyeko ziarani kikazi Washington DC amekuwa na mazungumzo na Iyad Ameen Madani ambaye ni Katibu Mkuu wa Ushirikiano wa nchi za kiislamu, OIC.

Wawili hao wamejadili mchakato wa amani Mashariki ya kati pamoja na hali nchini Iraq, Yemen na Syria ambapo Ban amemwomba Bw. Madani ushirikiano wake katika kushughulikia masuala hayo.

Halikadhalika Ban amezungumzia maswala hayo hayo alipokutana na na Katibu Mkuu wa Umoja wa nchi za kiarabu, Nabil El-Araby, wakizingatia umuhimu wa kuongeza juhudi za kimataifa ili kupambana na ugaidi.

Katibu Mkuu pia amekutana na waziri wa mambo ya nje wa Chad, Moussa Faki Mahamat na kuongea naye kuhusu masuala ya usalama hususan kutandaa kwa kundi la Boko Haram katika maeneo ya ziwa Chad.