Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UM wapongeza ziara ya kiongozi wa Kurdistan nchini Iraq

UM wapongeza ziara ya kiongozi wa Kurdistan nchini Iraq

Mwana diplomasia wa Umoja wa Mataifa nchini Iraq amepongeza tukio la ziara ya kiongozi wa Kurdish Masoud Barzani,aliyezuru Baghdad kwa maelezo kuu kitendo hicho kinafungua ukurasa mpya wa kiasiasa na hivyo kuweka mwanga wa kuwa na majadiliano ya mezani kwa ajili ya kusaka suluhu ya mikwamo inayojitokeza katika eneo hilo.Martin Kobler,ambaye ni mwakilishi maalumu wa Katibu Mkuu nchini Iraq amesema kuwa ametiwa moyo na hatua ya rais wa Kurdistan kuwa na ziara nchini humo ambako amekutana na kuwa na mazungumzo na Waziri Mkuu Nuri al-Maliki, Spika wa bunge Osama al-Nujaifi na maafisa wengine wa serikali.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, Kobler amesema kuwa ziara hiyo ni kitendo kinacho ashiria kuwepo kwa utashi wa kisiasa na hivyo pande hizo sasa zipo tayari kutafuta suluhu ya mikwamo inayojitokeza kwa njia ya majadiliano ya mezani.

Ziara ya kiongozi huyo inakuja katika kipindi cha mwezi mmoja tangu Waziri Mkuu wa Iraq kuwa na ziara ya kwanza katika historia ya uhusiano wa mataifa hayo mawili, ambako alikuyana na kufanya mazungumzo na viongozi wa Kurdistan.