Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kundi la BRICS lazidi kushamiri kwenye uwekezaji wa nje

Kundi la BRICS lazidi kushamiri kwenye uwekezaji wa nje

Ripoti mpya ya chombo cha kufuatilia mwelekeo wa uwekezaji duniani, GITM imedhihirisha ongezeko la vitegauchumi vya kigeni duniani hususan barani Afrika kutoka kundi la nchi za BRICS ambazo ni Brazil, Urusi, Afrika Kusini, China na India.

Ripoti hiyo iliyotolewa leo siku moja kabla ya kuanza kwa mkutano wa viongozi wakuu wa BRICS huko Durban Afrika Kusini kuhusu ubia kati ya BRICS na bara la Afrika yaonyesha kuwa vitegauchumi vya nchi hizo kwa bara hilo vimeongezeka na vimejikita zaidi katika sekta ya uzalishaji na huduma badala ya mafuta na madini. Mathalani mwaka 2012 uwekezaji huo kwa Afrika ulikuwa asilimia 25.

Halikadhalika kidunia, katika muongo mmoja uliopita, uwekezaji wa moja kwa moja kutoka BRICS uliongezeka mara tatu zaidi na kufikia dola Bilioni 263 mwaka 2012 na kufanya kiwango cha ushiriki wa  nchi hizo kwenye uwekezaji wa kigeni kuwa asilimia 20 mwaka jana ikilinganishwa na asilimia Sita mwaka 2000.