Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Rushwa yapokonya wengi haki za binadamu :Pillay

Rushwa yapokonya wengi haki za binadamu :Pillay

Kamishina Mkuu wa haki za binadamu kwenye Umoja wa Mataifa Navi Pillay amesema kuwa hamna shaka kwamba ulaji rushwa ni kizingiti kikubwa katika kuwepo kwa haki za binadamu  zikiwemo za kisiasa , kiuchumi , kijamii , kitamaduni na maendeleo.  Pillay amesema ulaji rushwa unakiuka haki muhimu za kibinadamu zikiwemo za uwazi , uwajibikaji , kutobaguliwa na kukosa kushirikishwa kwenye masuala ya kijamii. Amekieleza kikao cha Baraza la Haki binadamu mjini Geneva kuwa ulaji rushwa sio tu tatizo la maeneo fulani au jamii fulani na haupo tu kwenye ofisi za umma lakini pia kwenye sekta ya biashara na  michezo kote duniani.  Inaripotiwa kuwa tangu mwaka 2000 hadi 2009 nchi zinazoendelea zilipoteza dola trillioni 8.44 kwenye masuala ya kifedha yaliyo kinyume na sheria.

 (SAUTI YA Pillay)

“Ulaji rushwa unaua, Pesa zinazoibwa kupitia ulaji rushwa kila mwaka zinatosha kuwalisha walio na njaa duniani mara 80 zaidi. Karibu watu milioni 870 hulala njaa kila siku wengi wakiwa ni watoto, ulaji rushwa huwanyima haki yao wa kupata chakula na mara nyingine haki yao ya kuishi. Utoaji rushwa na wizi unagharimu miradi inayoweza kutoa maji safi ya kunywa na usafi kote duniani hadi asiliamia 40. Pesa zinazoibwa kutoka kwa serikali zingeweza kutumiwa kwenye maendeleo kuwahakikishia watu madawa na kuzuia mamia ya vifo vya kila siku  vitokanavyo na uja uzito na wakati wa kujifungua.”